Bodi ya TPDC yaridhishwa na maendeleo ya mradi wa kituo cha ujazaji gesi Mlimani

Mtanzania
Published: Mar 03, 2025 11:31:02 EAT   |  News

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Diogital Mwakilishi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Paul Makanza, ameongoza ukaguzi wa maendeleo ya mradi wa kituo mama cha ujazaji gesi asilia kilichopo Mlimani, Dar es Salaam, ambapo ameonesha kuridhishwa na hatua iliyofikiwa. Akizungumza leo, Machi 3, 2025, baada ya ziara hiyo, Makanza alisema […]

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Diogital

Mwakilishi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Paul Makanza, ameongoza ukaguzi wa maendeleo ya mradi wa kituo mama cha ujazaji gesi asilia kilichopo Mlimani, Dar es Salaam, ambapo ameonesha kuridhishwa na hatua iliyofikiwa.

Akizungumza leo, Machi 3, 2025, baada ya ziara hiyo, Makanza alisema kuwa mradi huo ni muhimu kwa sababu gesi asilia iliyokandamizwa (CNG) ni mbadala wa mafuta, hatua inayosaidia nchi kuokoa fedha za kigeni na kuboresha uchumi.

“Tumeridhika kama Bodi kwa maendeleo ya mradi huu. Unapokuwa mkubwa, faida zake zitakuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa taifa kwa kupunguza utegemezi wa mafuta ya petroli,” amesema Makanza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa TPDC, Derick Moshi, alisema kuwa ujenzi wa kituo hicho umekamilika kwa zaidi ya asilimia 90, huku hatua za mwisho zikiwa ni ukaguzi wa mifumo ya usalama kabla ya kuanza majaribio rasmi.

“Kituo kimeshakamilika kwa kiwango kikubwa, na gesi tayari ipo. Tunachosubiri kwa sasa ni majaribio kwa magari, ambayo tunatarajia yataanza kabla ya mwisho wa mwezi huu,” amesema  Moshi.

Katika juhudi za serikali kukuza matumizi ya nishati TPDC imeeleza kuwa inatekeleza mpango wa kupanua mtandao wa vituo vya ujazaji gesi kwenye magari. Kwa sasa, vituo saba vipya vipo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kupunguza gharama za mafuta kwa wananchi na kusaidia sekta ya usafirishaji.