TCU yaanza mapitio ya mitaala 300 ya vyuo vikuu nchini

Mtanzania
Published: Feb 23, 2023 06:45:14 EAT   |  Educational

Na Ramadhan Hassan, Dodoma Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imesema mitaala 300 ya vyuo vikuu inafanyiwa mapitio ili kuhuishwa kwa kuzingatia maoni ya wadau mbalimbali ili kukidhi matarajio yao na mahitaji ya soko. Katibu Mtendaji wa tume hiyo, Profesa Charles Kihampa amesema hayo Jumatano Februari 22,2023 jijini Dodoma wakati akielezea utekelezaji wa shughuli za […]

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imesema mitaala 300 ya vyuo vikuu inafanyiwa mapitio ili kuhuishwa kwa kuzingatia maoni ya wadau mbalimbali ili kukidhi matarajio yao na mahitaji ya soko.

Katibu Mtendaji wa tume hiyo, Profesa Charles Kihampa amesema hayo Jumatano Februari 22,2023 jijini Dodoma wakati akielezea utekelezaji wa shughuli za TCU.

Amesema TCU imeendelea kuandaa na kuratibu mafunzo kwa viongozi, wahadhiri na maofisa wa vyuo vikuu vya umma na binafsi hapa nchini kwa lengo la kuwajengea uwezo katika usimamizi na uendeleshaji wa taasisi zao.

Ametoa mfano kuanzia mwaka 2022/2023, Serikali imetenga Sh Trilioni 6.4 kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) kwa ajili ya kuimarisha uthibiti ubora na uhuishaji wa mitaala ya vyuo vikuu.

“Zaidi ya mitaala 300 ya vyuo vikuu iko katika hatua mbalimbali za kufanyiwa mapitio ili kuhuishwa kwa kuzingatia maoni ya wadau mbalimbali iki kukidhi matarajio yao na mahitaji ya soko,”amesema.

Aidha, Profesa Kihampa amesema maboresho ya mifumo yameongeza tija na ufanisi na kurahisisha utoaji wa huduma kwa kuwawezesha wananchi na wadau mbalimbali kupata huduma bora na kwa haraka.

Ametoa mfano muda wa uhakiki na utambuzi wa tuzo za nje ya nchi umepungua kutoka siku 14 za awali hadi siku tatu.

“Pia waombaji wa udahili wanaweza kutuma maombi yao moja kwa moja kwenye vyuo husika na kuthibitisha vyuo wanavyopenda popote walipo bila kulazimika kusafiri kwenda chuoni,”amesema.