Sisalana wapigia chapuo bidhaa za mkonge

Mtanzania
Published: Dec 13, 2022 18:19:00 EAT   |  Travel

Na Norah Damian, Mtanzania Digital Kampuni Sisalana inayomilikiwa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) imeongeza thamani ya kilimo cha mkonge kwa kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo zimeleta mageuzi sokoni. Kampuni hiyo yenye makao yake makuu mkoani Tanga inazalisha bidhaa za mkonge kama vile kamba, mazulia, mikoba na nyingine. Akizungumza juzi kwenye Maonesho ya […]

Na Norah Damian, Mtanzania Digital

Kampuni Sisalana inayomilikiwa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) imeongeza thamani ya kilimo cha mkonge kwa kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo zimeleta mageuzi sokoni.

Kampuni hiyo yenye makao yake makuu mkoani Tanga inazalisha bidhaa za mkonge kama vile kamba, mazulia, mikoba na nyingine.

Akizungumza juzi kwenye Maonesho ya Saba ya Bidhaa za Viwanda vya Tanzania yaliyofanyika Uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere maarufu Sabasaba, Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Elizabeth Kalambo, amesema wamepata mwitikio mkubwa kutoka kwa Watanzania.

“Hii ni mara yetu ya tatu tunashiriki katika maonesho haya, tunashukuru kwa mwitikio ambao tumeupata na tunazidi kutoa Wito kwa Watanzania kupenda bidhaa za Tanzania kwa sababu unapotumia bidhaa ya Tanzania unajenga nchi yetu,” alisema Elizabeth.

Alisema pia wanatafuta mawakala ambao watauza bidhaa zao sehemu mbalimbali ili waendelee kumuongezea thamani mkulima na kumpatia kipato kikubwa.

Katika maonesho hayo kampuni hiyo pia ilizawadiwa cheti cha ushiriki kilichotolewa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (Tantrade).

Maonesho hayo yaliyoanza Desemba 3,2022 na kuhitimishwa Desemba 9,2022 yalikuwa na washiriki 502 na yaliongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Nunua bidhaa za Tanzania jenga Tanzania’.