NMB yazindua ‘Elimu Loan’ kuwakopesha wafanyakazi kupata elimu

Mtanzania
Published: Mar 15, 2023 06:27:39 EAT   |  Educational

Na Beatrice Kaiza, Mtanzania Digital Benki ya NMB imetenga Sh bilioni 200 kwa ajili ya kuwakopesha wafanyakazi kupata elimu ya juu au wale wanaohitaji fedha za kuwasomesha wategemezi wao. Huduma hio mpya ya mikopo ya elimu ya juu ‘NMB Elimu Loan’ yenye riba nafuu maalum kwa ajili ya watumishi na wafanyakazi ambao mishahara yao inapitia […]

Na Beatrice Kaiza, Mtanzania Digital

Benki ya NMB imetenga Sh bilioni 200 kwa ajili ya kuwakopesha wafanyakazi kupata elimu ya juu au wale wanaohitaji fedha za kuwasomesha wategemezi wao.

Huduma hio mpya ya mikopo ya elimu ya juu ‘NMB Elimu Loan’ yenye riba nafuu maalum kwa ajili ya watumishi na wafanyakazi ambao mishahara yao inapitia benki ya NMB imezinduliwa leo jijini Dodoma machi 14,2023.

Kwa mujibu wa benki hiyo huduma hiyo italeta ahueni kubwa katika ufadhili wa elimu ya juu nchini na pia itatolewa kwa vyuo vya kati ikiwemo vyuo vya ufundi.

Akitangaza mpango huo Machi 14, mwaka huu jijini Dar es Salaam, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna amesema mpango huo wa mkopo unaotolewa kwa mwajiriwa yeyote ambae ni mteja wa NMB unaanzia Sh 200,000 hadi Sh milioni 10 kwa mwaka kwa mtu mmoja ambapo riba itakuwa asilimia 9 na muda wa marejesho ni hadi miezi 12.

Mkopo huo pia utatolewa kwa ngazi ya vyuo vya kati vikiwamo vile vya ufundi.

“Huu ni utekelezaji wa makubaliano yetu na Wizara ya Elimu ya kuanza kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa ajili ya kupunguza utegemezi wa waajiriwa kwa bodi ya mikopo (HESLB) pale wanapotaka kujiendeleza kimasomo na pia kuwalipia ada vijana wao.

“NMB ina dhamira ya dhati katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha tasnia ya elimu na kuchangia kutoa elimu bora kwa wote huku ikiwa mstari wa mbele kupanua wigo wa upatikanaji wa fedha za kuwafadhili wote wanaohitaji kujiendeleza kielimu.

“Ili kupata mkopo huu, fika tawi lolote la NMB na nakala ya mshahara wako, mtiriko wa ada, barua ya kujiunga na chuo na wafanyakazi wa Benki ya NMB watakupigia hesabu ya mkopo unaostahili kupata,” amesema Zaipuna.

Kwa kuanzisha huduma hii, NMB inakuwa imetimiza ahadi iliyoitoa mwaka jana yakuisaidia Serikali kuipunguzia HESLB mzigo wa kufadhili masomo ya juu na kuwa na vyanzo vipya vya mikopo ya elimu.

Upande wake Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda ameweka wazi kiu yake ya kuona upatikanaji wa ufadhili zaidi ya kile ilichokifanya NMB kutoka kwa wadau wengine.

Aidha, amesema kuwa uwekezaji wa NMB ni kitu kikubwa kinachoongeza wigo wa watu kujisomesha na akaomba hela za mikopo hiyo zitumike kwa ajili ya madhumuni yaliyokosudiwa tu.