Hazina Saccos kupunguza Riba mwaka 2022

Mtanzania
Published: Dec 13, 2021 14:17:36 EAT   |  News

Na Ramadhan Hassan,Dodoma CHAMA cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Hazina (Hazina SACCOS) kimesema kimejipambanua kuwa na mlengo wa kutoa huduma kulingana na mahitaji na changamoto zinazowakabili wanachama ambapo mwaka 2022 wanatarajia kupitia upya riba ili kuweza kupunguza. Hayo yameelezwa leo Jumatatu Desemba 13, jijini Dodoma na Kamishna Msaidizi kutoka Wizara ya Fedha na […]

Na Ramadhan Hassan,Dodoma

CHAMA cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Hazina (Hazina SACCOS) kimesema kimejipambanua kuwa na mlengo wa kutoa huduma kulingana na mahitaji na changamoto zinazowakabili wanachama ambapo mwaka 2022 wanatarajia kupitia upya riba ili kuweza kupunguza.

Hayo yameelezwa leo Jumatatu Desemba 13, jijini Dodoma na Kamishna Msaidizi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Jonesia Mjema, wakati akizungumza mkutano mkuu wa nane wa Wawakilishi wa Hazina Saccos Ltd.

Kamishna huyo amesema Hazina Saccos imejipanga kuwa chama chenye mlengo wa kutoa huduma kulingana na mahitaji na changamoto zinazowakabiliwa wanachama.

Amesema mwaka 2022 wanatarajia kupitia upya riba ili kuweza kupunguza.

Aidha, amesema wanatarajia kuongeza kiwango cha kukopa mikopo ya dharura kwa wanachama kutokaSh milioni 2 hadi Sh milioni 5.

Amesema changamoto ambazo wanakutana nazo ni pamoja na makato makubwa ya michango ya kila mwezi pamoja na marekebisho ya mikopo.

“Hazina Saccos kwa sasa inatoza asilimia 12 ‘reducing balance’ kwa mwaka kwenye mikopo inayotoa kwa wanachama wake. Hazina Saccos inalipa asilimia 24 kwa mwaka ‘straight line’ kama gharama za makusanyo ya michango ya wanachama pamoja na marejesho ya akiba,”amesema Mjema.

Amesema changamoto zingine ni upatikanaji wa leseni ya kuendeshea chama,udogo wa chumba cha ofisi Mkoani Dodoma pamoja na uwekaji hafifu wa akiba kwa wanachama ambapo amedai wengi wanachangia akiba ndogo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Hazina Saccos, Aliko Mwaiteleke amesema  mpaka sasa wana maeneo zaidi ya manne katika Jiji la Dodoma ambayo wameyachukua na kuyapima na wamewapatia  viwanja wanachama.

Ameyataja maeneo hayo na idadi ya viwanja katika mabano  kuwa ni Ihumwa Ngaloni (430), Iyumbu (360),Nzuguni (106) na Ihumwa Ilolo (340).

 “Tunachoangalia  sisi wanachama wetu tunawauzia kwa bei ya chini baada ya kuwapa ni hiari yao kujenga na tunaona wanajenga sana na sisi tumeunga mkono Serikali kuhamia Dodoma,”amesema Mwaitekela.

Mwenyekiti huyo wa Bodi amesema wao wapo kwa ajili ya kuhudumia wanachama ambapo wameingiza zaifdi ya wanachama 600 kwa mwaka ambapo lengo lilikuwa ni kuingiza wanachama 500.

“Sisi kama chama ni kuhaklikisha tunajipambambanua kama chama cha kusaidia watumishi wa umma,mpaka sasa tumekusanya akiba za wanachama bilioni 15 hisa ni 1.2 bilioni jumla ya mali za chama ni bilioni 18.

“Tunaamini ukuaji wa chama ni mkubwa na wengi wanafaidika niwatumishi wote.Kwenye vyama uadilifu unahitajika sana.

“Sisi ndani ya chama  ukiangalia Bodi na uanachama kwenye eneo la ukopaji hakuna mwenye upendeleo na hakuna mwenye haki zaidi ya mwanachama mwingine.Uwazi kwetu ni mkubwa sana na sisi tumeimarisha mifumo,”amesema.

Naye, Naibu Mrajis wa Vyama vya Ushirika Nchini, Collins Nyakunga amesema uwepo wao katika mkutano huo ni kuhakikisha  taratibu na kanuni zinazoongoza ushirika zinafuatwa.

“Tuna jukumu la kuhakikisha wenzetu hawa wanazingatia sheria na taratibu zinazoongoza ushirika sisi jukumu letu ni kuangalia ni namna gani wanafanya na pale watakapoenda kinyume na taratibu hatuna mamlaka ya kuingilia maamuzi yao.

“Lakini ni kuwarudisha kwenye mstari nini wanatakiwa wafanye kuhakikisha kwamba wanachama wanafurahia kuwa katika Saccos hiyo,”amesema.