Aliyedanganywa na shetani atupwa jela miaka 30 na viboko 12

Mtanzania
Published: May 31, 2023 22:08:23 EAT   |  General

*Ni baada ya kukiri kumbaka mtoto wa miaka 13 Na Malima Lubasha, Bunda MKAZI wa Mtaa wa Luselu katika mji wa Bunda mkoani Mara, Masubugu Masubugu (32) amehukumiwa kwenda jela miaka 30, kuchapwa viboko 12 na kulipa fidia Sh milioni moja baada ya kutiwa kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka 13 mwanafunzi wa shule […]

*Ni baada ya kukiri kumbaka mtoto wa miaka 13

Na Malima Lubasha, Bunda

MKAZI wa Mtaa wa Luselu katika mji wa Bunda mkoani Mara, Masubugu Masubugu (32) amehukumiwa kwenda jela miaka 30, kuchapwa viboko 12 na kulipa fidia Sh milioni moja baada ya kutiwa kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka 13 mwanafunzi wa shule ya msingi Nyambitirwa.

Hukumu hiyo imetolewaMei 30, 2023 na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Bunda, Mulokozi Kamuntu baada ya mshtakiwa kukiri kosa.

Awali, Mwendesha mashtaka wa Serikali kutoka Jeshi la polisi D/Sgt Athuman Salimu alidai kuwa mshtaki wa  Masubugu alitenda kosa hilo Mei 23, mwaka huu saa 8.00 mchana eneo la mtaa wa Luselu ndani ya mji wa Bunda.

Imeelezwa mahakamani hapo kuwa, Masubugu, alimkamata kwa nguvu mtoto huyo na kumuingiza kwenye nyumba ya nyasi kisha kumbaka baada ya kumaliza unyama huo alitoka na kukimbia kusikojulikana.

Mtoto huyo (jina limehifadhiwa) alitoka na kwenda kutoa taarifa kwa wazazi na kupelekwa kituo cha polisi na baadaye hospitali kwa matibabu na kufanyiwa uchunguzi wa afya yake.

“Jeshi la polisi lilifanikiwa kumkamata Masubugu na kumfikisha mahakamani,” amedai D/Sgt Salim.

Awali, baada ya kukumbushwa mashtaka yanayomkabili, Masubugubu alijbu kuwa ni kweli alifanya kitendo hicho na ndipo mahakama ilipomtia hatiani kwani hakuisumbua mahakama.

Baada ya mshtakiwa kutiwa hatiani mwendesha mashtaka aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshtakiwa kwa maelezo kuwa matukio hayo ya kinyama yamekithiri katika jamii na kuharibu saikolojia ya watoto ambao ni viongozi wa kesho na ili liwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama yake.

Katika utetezi wake, Masubugu aliiomba mahakama kumpunguzia adhabu kwa kuwa alipitiwa na kwamba shetani ndiye alimdanganya.

Hata hivyo utetezi huo ulitupiliwa mbali na mahakama, ndipo Hakimu Kamuntu alipomhukumu kwenda jela miaka 30, kuchapwa viboko 12 na kulipa fidia Sh 1,000,000.

“Kutokana na ushahidi uliowasilishwa pamoja na wewe mwenyewe kukili kosa, mahakama inakuhukumu kwenda jela miaka 30, sambamba na kuchapwa viboko 12, sita wakati wa kuingia na sita wakati wa kutoka, pia utatakiwa kulipa fidia ya Sh milioni moja,” amesema Hakimu Kamuntu.