Fei Toto akata kilo sita Azam

KIUNGO fundi wa soka anayekipiga Azam FC, Feisal Salum ‘Fei Toto’ amekiri wakati anajiunga na timu hiyo alikuwa chibonge, lakini kwa sasa amejitahidi kupambana hadi kukata zaidi ya kilo sita na kujiona mwepesi na kuanza kurejesha makali aliyokuwa nayo enzi akiitumikia Yanga. Fei Toto amejiunga na Azam msimu huu baada ya kuuzwa kutoka Yanga aliyoifanyia mgomo tangu mwishoni mwa Desemba mwaka jana kabla ya Rais Samia Suluhu Hassan kuingilia kati kwenye hafla ya kuipongeza timu hiyo ya Jangwani kwa kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu uliopita. Kiungo huyo aliyasema hayo kwenye mahojiano maalumu na Mwanaspoti akisema awali alipojiunga Azam alikuwa na uzito wa kilo 75, lakini baada ya kupigishwa tizi la maana kwa sasa amebaki na kilo 69 na kujiona mwepesi na kurejea kwenye ule utamu uliompa mashabiki akiwa na Yanga aliyoichezea misimu minne. Fei alisema wakati anaanza kucheza alipata wakati mgumu sana, kwani alikuwa kibonge ila anamshukuru sana kocha kwani alimsaidia mno na kumrejeshea katika hali ya kuwa fiti. “Timu ilinipatia mkufunzi maalum wa kunifundisha mazoezi binafsi yalinisaidia kurudi katika hali, kwani nilikaa nje karibu miezi minne bila kucheza na kwa bahati nimepunguza uzito na sasa nimeanza kurejea katika makali niliyokuwa nayo Yanga,” alisema Fei Toto aliyewahi kuichezea JKU na kutua kwa muda Singida Utd. Kiungo huyo alifunga mabao matatu katika mechi ya kwanza wa Ligi Kuu dhidi ya Tabora United iliyokuwa na wachezaji pungufu.