NMB kuendelea kuipiga jeki Serikali sekta ya elimu nchini

Mtanzania
Published: Oct 21, 2022 14:17:31 EAT   |  Educational

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital Benki ya NMB imeeleza kuwa imekuwa ikiwajibika kwa jamii kila mwaka ikiwa ni sehemu ya kusaidiana na Serikali juhudi za kuweka mazingira bora ya kufundishia na kusomea kwa kutoa msaada wa vifaa vya elimu katika shule za msingi na sekondari hapa nchini. Akizungumza katika mahafali ya 62 ya shule ya […]

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Benki ya NMB imeeleza kuwa imekuwa ikiwajibika kwa jamii kila mwaka ikiwa ni sehemu ya kusaidiana na Serikali juhudi za kuweka mazingira bora ya kufundishia na kusomea kwa kutoa msaada wa vifaa vya elimu katika shule za msingi na sekondari hapa nchini.

Akizungumza katika mahafali ya 62 ya shule ya sekondari ya wanafunzi wenye vipaji maalumu ya Mzumbe mkoani hapa, Mkaguzi Mkuu wa Ndani Benki ya NMB, Benedicto Baragomwa amesema benki hiyo imekuwa ikitoa vifaa mbalimbali sekta ya elimu kila mwaka hapa nchini ili kusaidiana na serikali katika kuboresha sekta hiyo.

Baragomwa amesema benki hiyo imekabidhi viti 50 na meza 50 vyenye thamani ya sh5milioni shule ya sekondari Mzumbe katika mahafali hayo ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa meza na viti kwa wanafunzi darasani.

“NMB imekuwa ikishirikiana na serikali katika kuweka mazingira bora ya kusomea na kufundishia sekta ya elimu nchini na hapa leo Mzumbe sekondari tumekabidhi viti 50 na meza 50 ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa vifaa hivyo na tupo katika mipango ya kuleta kompyuta hapa.”amesema Baragomwa.

Kaimu Mkuu wa shule ya sekondari Mzumbe, Edwin Matenga amesema shule hiyo imekuwa ikishika nafasi tofauti tofauti katika shule 10 bora za sekondari katika matokeo ya kidato cha pili, nne na sita.

“Wanafunzi katika matokeo ya mitahani ya taifa kidato cha pili, nne na sita imekuwa ikifanya vizuri kwa kuwa katika shule 10 bora kwa shule za sekondari binafsi na serikali na tunashukuru benki ya NMB kutoa msaada ya viti 50 na meza 50 kwa kutufadhili na umesaidia kuondoa changamoto kubwa ya thamani hizi,” amesema Matenga.

Matenga amesema licha ya mafanikio ya kitaalumu lakini kumekuwa na changamoto ya miundombinu kuchoka ikiwemo vyoo, uchakavu wa nyumba za watumishi na kipindi cha masika kuwa na wasiwasi.

Mkuu wa mkoa wa Tanga, Omari Mgumba ambaye ni mmoja wa wazazi wa wanafunzi wanaotarajia kuhitimu elimu ya sekondari katika shule hiyo mwaka huu amesema baada ya kumalizika kwa mahafali hiyo wanafunzi wana wajibu sasa wa kufanya maandalizi kwa ajili ya mitihani ya taifa kidato cha nne.

“Nimekuja kwenye haya mahafali Mzumbe sekondari kama mzazi na niwapongeze uongozi wa benki ya NMB kutumia mahafali hayo kutoa msaada wa viti na meza na hii ni fahali kwa serikali taasisi hii inaposaidia kutoa vifaa vya elimu katika shule za sekondari na msingi hapa nchini,” amesema Mgumba.