Jela kwa kujifanya Usalama wa Taifa

Milard Ayo
Published: May 25, 2023 13:13:20 EAT   |  General

Mahakama ya wilaya ya Babati mkoa wa Manyara imemhukumu Patrick Wambura (34) mkazi wa Bariadi Mkoani Simiyu kutumikia kifungo cha miezi mitatu gerezani kwa kosa la kujifanya Ofisa usalama wa Taifa. Hukumu hiyo imetolewa leo na Hakimu mkazi Mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Babati Victor Kimario ambapo amesema mshtakiwa huyo alijitambulisha kwa Ofisa wa […]

Mahakama ya wilaya ya Babati mkoa wa Manyara imemhukumu Patrick Wambura (34) mkazi wa Bariadi Mkoani Simiyu kutumikia kifungo cha miezi mitatu gerezani kwa kosa la kujifanya Ofisa usalama wa Taifa.

Hukumu hiyo imetolewa leo na Hakimu mkazi Mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Babati Victor Kimario ambapo amesema mshtakiwa huyo alijitambulisha kwa Ofisa wa Baraza la ardhi na nyumba wilaya ya Babati Januari 18 mwaka jana kuwa yeye ni Ofisa usalama wa Taifa.

Amesema mshtakiwa huyo alijiita Ofisa usalama wa Taifa akidai anafatilia nyaraka za kesi ya Mlale Sogweda ambaye alikuwa na shauri katika Baraza hilo.

Hakimu Kimario amesema upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi wanne na vielelezo vitano, huku hoja iliyoifanya mahakama kukubaliana na ushahidi huo ni kuwa mashahidi waliiambia mahakama kuwa mshtakiwa alikuwa anaonekana mahakamani mara kwa mara akijifanya kuwatetea watu wakati akijua yeye siyo wakili.

Kimario amesema shahidi namba moja, mbili na tatu walisema kuwa mshtakiwa alienda pale ofisini mchana na kujitambulisha kuwa ni Ofisa usalama wa Taifa,huku shahidi namba nne ambaye ni askari polisi ndio alioneshwa kuwa mhusika ni huyo na baada ya kutoka pale alikamatwa na kufikishwa kituo cha polisi Babati na alipopekuliwa alikutwa na kitambulisho cha Taifa tu.

“Kitendo alichokifanya Wambura siyo kizuri cha kujipendekeza na kujifanya mtu mashuhuli katika jamii hivyo nakutia hatiani uende gerezani ukatumikie miezi mitatu,”amesema Kimario

Awali kabla ya hukumu hiyo mwendesha mashtaka wa serikali Mwanaidi Chuma aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa kosa alilolifanya,huku Mshtakiwa akiiomba mahakama kumuondolea adhabu hiyo kwa kuwa ana mtoto mdogo wa miezi minne na watoto wengine wanne ambao ni yatima mama yao alishafariki na yeye mwenyewe ni mgonjwa hivyo anaomba apunguziwe adhabu.